TADB yafufua kiwanda cha pamba Kahama
Na Abdallah Luambano, Kahama
NAIBU Waziri wa Kilimo, Bw. Hussein Bashe amezindua kiwanda cha pamba cha kahama (KACU) kilichofufuliwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) ambapo zaidi ya shilingi bilioni 4.6 zimeshatolewa na benki. Akizungumza katika uzinduzi huo mjini hapa jana, Bw. Bashe alisema kufufuliwa kwa kiwanda hicho ni dhamira ya kweli ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuinua na kuongeza uzalisha wa mazao yote ya kimkakati ikiwepo pamba hapa nchini.
“Kuzinduliwa kwa kiwanda hiki leo (jana) inamaana kubwa sana kwa wakulima wa pamba kwa maeneo hayo kwani kitasaidia kuongeza uzalishaji wa pamba na kuwaongezea kipato wakulima wa zao hili,’’ alisema.
Alisema kutokana na umuhimu wa kiwanda hicho alilazimika kuhamishia ofisi yake TADB ili kuhakikisha zoezi la kukifufua kiwanda linakamlika kwa wakati na kuleta mapinduzi ya dhahabu nyeupe(pamba).
“Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza benki ya TADB na mabenki washirika wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mrajisi wa Ushirika na wengine kwa namna mlivyosimamia kukamilika kwa zoezi la kufufua kiwanda hiki ambacho kitawanufaisha wakulima mkoani Shinyanga,’’ alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Japhet Justine alisema sema uzinduzi wa kiwanda hicho cha pamba utaongeza tija kwa wakulima kwa kuwa bei ya pamba itaongezeka na kuwafanya wamudu gharama za maisha na kuchangia ukuaji wa pato la Taifa.
“Uzinduzi wa kiwanda hiki utaongeza uzalishaji wa pamba ambayo ni malighafi muhimu kwa viwanda vya ndani lakini thamani ya zao la pamba litaongezeka na kuzidi kutoa mchango wake katika ukuaji wa pato la Taifa na mkulima mmoja mmoja,’’ alisema Bw. Justine.
Bw. Justine alisema vyama vya ushirika kupitia vyama vya ushirika wa kilimo na masoko ( AMCOS) vinakopesheka na kutoa wito kwa wakulima kujiunga na navyo iliwaweze kufaidika na huduma za benki yake kwa karibu.
“Sisi kama benki ya kilimo tunaamini kuwa kilimo kinakopesheka kwa kuwa tumefanya hivyo sehemu mbalimbali ikiwemo hapa kahama, tunatoa wito kwa wakulima kujiunga kwenye hizo AMCOS ili waweze kukopeshwa kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa zao la pamba,’’ alisema.
Aliongeza kuwa licha ya bei ya zao la pamba kushuka thamani tangu kufungwa kwa kiwanda cha pamba cha kahama kwa msimu wa 2013/14, sasa kufufuliwa kwa kiwanda hicho kutarejesha matumaini mapya kwa wakulima wa zao hilo mkoani Shinyanga.
“Mbali ya kufufua kiwanda hiki ambacho kilisimamisha uzalishaji wake tangu msimu wa 2013/14, tumefanya juhudi kubwa kurejesha uzalishaji wa zao hilo na kwa msimu huu tumenunua kilo ya pamba kwa shilingi kati ya 800 mpaka 920,’’ alisema na kuongeza kuwa hilo ni jambo la kujivunia hasa katika kipindi hiki ambacho serikali inatekeleza azma yake ya ujenzi wa viwanda.
Bw.Justine mbali ya kuzishukuru taasisi mbalimbali pamoja na wadau waliochangia kukamilika kwa mpango huo, ameeleza kuwa kiwanda hicho kitawanufaisha wakulima zaidi 6,800 kutoka AMCOS 79 jambo ambalo litaongeza tija kwa wakulima na Taifa kwa ujumla.
Comments
Post a Comment