Simbachawene: Serikali itaendelea kusimamia matumizi ya chuma chakavu


Na Mosses Mahundi, Dar es Salaam

Serikali imesema jana kwamba itaendelea  kusimamia kwa karibu sana kuwepo na matumizi ya  vyuma chakavu na taka hatarishi kwa sababu vitu hivyo  moja ya rasilimali muhimu sana katika kutekeleza azma ya serikali ya kujenga uchumi wa kati na viwanda ifikapo 2025.

Kauli hii imetolewa Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Bw George Simbachawene, alipotembelea Kiwanda ch OK Plast cha Dar es Salaam ambako ameelezwa kwamba kiwanda hicho kinatumia chuma chakavu na taka hatarishi kama malighafi ya kutengeneza nyaya za shaba na kinatumia betri za magari chakavu kutengeneza  mikeke ya kisasa.

Akizungumza na wafanyakazi na viongozi wa kiwanda hicho, Waziri Simbachawene amesema serikali itaendelea kusimamia kwa karibu marufuku ya usafirishaji wa chuma chakavu na taka hatarishi  ili vitumiwe na viwanda vya ndani kutengeneza bidhaa kwa soko la ndani na nje.

“Nawashukuru nyinyi OK Plast, kwa sababu  mmeonyesha kwa nini serikali ilifanya maamuzi ya kuzuia usafirishaji wa chuma chakavu na taka hatarishi nje ya nchi. Viwanda vya ndani ni muhimu sana katika kutoa nafasi za ajira, lakini pia tutasafirisha bidhaa hizo nje kama ambavyo OK Plast mnafanya. Hali hiyo itatuingizia pesa za kigeni na kuongeza thamani ya pesa yetu hapa nchini,’’ ameieleza hafla hiyo.

Amesema kuwa ushahidi mwingine wa thamani ya marufuku hiyo ni kwamba  chuma chakavu na taka hatarishi vinavyopatikana nchini bado vinahitajika mno kwani hivyo vinavyopatikana havitoshelezi mahitaji ya viwanda vya ndani.

“Duniani kote sasa wanatumia malighafi hizi za vyuma chakavu na taka hatarishi katika kujipatia malighafi za viwanda vyao. Hivyo nasi hatuna budi kurejeleza vyuma hivyo ili vitumike kama malighafi katika viwanda vya ndani,” amewaeleza wafanyakazi na kuongeza  kuwa serikali iko makini na jambo hilo kwa sababu viwanda vya ndani vinachangia ukuaji wa pato la taifa

Akijibu ombi la  Afisa Mhakiki wa Kiwanda hicho, Bw.Anacleto Pereira, kwamba serikali itafute njia nzuri ili kiwanda chao kipate shaba kutoka kwa wachimbaji wadogo wa shaba nchini, waziri amewashauri  wenye viwanda vinavyotumia shaba katika kutengeneza bidhaa kuweka mipango yao vizuri ili wanunue shaba kutoka kwa wachimbaji wa ndani.

Bw Pereira ameishukuru serikali kwa kuweka marufuku hiyo na kueleza kwamba hapo nyuma kiwanda chao na vingine vilikuwa vinakabiliwa na uhaba wa malighafi hiyo wakati chuma chakavu na taka hatari vinapelekwa nje kuneemesha watu wengine.


Comments

Popular posts from this blog

Mkuu wa Mkoa Pwani asifu juhudi za mmiliki wa Makampuni ya Global Packaging na Wande Printing

17 projects to house 80,000 tonnes of crops being built

Tanesco: Azma ya uchumi wa kati na wa viwanda ifikapo 2025 inatekelezeka