Zungu ahadi akipa tano kiwanda cha nyaya za umeme

Waziri wa Nchi ofisi ya Makamu wa Rais(Muungano na Mazingira), Mussa Azzan Zungu(katikati) akiangalia baadhi ya bidhaa zinazozalishwa katika kiwanda cha Okplast kilichopo Jijini Dar es salaam ikiwa ni sehemu ya ziara yake kukagua hali ya utunzaji wa mazingira na pia kusikiliza kero za wawekezaji hao ili kuzifanyia kazi. Kushoto ni Afisa mazingira wa kiwanda hicho,Bw.Gilbert Grid na kulia ni Meneja wa Kanda ya Mashariki wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC),Anold Mapinduzi.
  

Waziri wa Nchi ofisi ya Makamu wa Rais(Muungano na Mazingira), Mussa Azzan Zungu(wapili kushoto) akiangilia shughuli zinazofanywa na na Kiwanda cha Okplast kilichopo Jijini Dar es salaam ikiwa ni sehemu ya ziara yake kukagua hali ya utunzaji wa mazingira na pia kusikiliza kero za wawekezaji hao ili kuzifanyia kazi. katikati ni Meneja wa Kanda ya Mashariki wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC),Anold Mapinduzi na Kulia ni Afisa mazingira wa kiwanda hicho,Bw.Gilbert Grid


Na Paul Mahundi, Dar es Salaam

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, (Muungano na Mazingira), Mussa Zungu amekipongeza kiwanda cha kuzalisha nyaya za umeme cha Ok Plast kwa kufanya uzalishaji unaozingatia kanuni na taratibu za mazingira na kuahidi kushughulikia changamoto ya uuzwaji wa taka za mabaki ya shaba nje ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam mara baada ya kutembelea kiwanda hicho, Waziri Zungu alisema kiwanda hicho kinafanya uzalishaji mkubwa wa nyaya za umeme ambazo soko l;ake kubwa lipo hapa nchini na kuahidi kushughulikia kero ambazo kiwanda hizo inakumbana nazo.

“Kiwanda kinafanya uzalishaji mzuri kwa kufuata kanuni na taratibu za mazingira, lakini wamekuwa na changamoto ya utunzaji wa taka baada ya kuyeyushwa kwa shaba ambayo kwa hapa nchini hazina soko. Nitaagiza timu ya wataalamu kuja kuangalia madhara yanayoweza kupatikana kwa kusafirishwa taka hizo nje ya nchi kabla ya kutoa kibali,’’ alisema Waziri Zungu.

Waziri alisema licha ya kushughulikia changamoto ya kiwanda hicho, amewataka wenye viwanda kote nchini kuacha kuhujumu miundombinu ya umeme, maji na madaraja kwa lengo la kupata malighafi za kuzalishia nyaya za umeme.

“Serikali ya awamu ya tano inatekeleza seraya uchumi wa viwanda. Utekelezaji wa azma hiyo lazima uende sambamba na utunzaji wa miudombinu yetu ya madaraja, umeme na maji. Natoa wito kwa wenye viwanda kuacha kuhujumu miundombinu ambayo serikali imetumia pesa nyingi za walipa kodi wa Tanzania kuijenga,’’ alisema.

Katika hatua nyingine amewataka wenye viwanda kuweka miundombinu rafiki katika kuhakikisha wanazuia kusambaa kwa hewa chafu ambayo imekuwa inazalishwa viwandani na hivyo kuleta athari kubwa kwa wakazi wa maeneo kuzunguka viwanda na pia kusababisha mabadiliko ya tabia nchi.

“Viwanda lazima vikidhi vigezo vya mazingira ikiwemo kutibu maji kabla ya kutitirishwa na namna nzuri ya kudhibiti hewa yenye ukaakaa ambayo imekuwa na athari hasi kwa viumbe hai pamoja na kusababishwa kwa mabadiliko ya tabia nchi,’’ alisema na kuongeza kuwa Wizara yake haitawavumilia wawekezaji wa aina hiyo.

Kwa upande wake Afisa Mazingira wa kiwanda hicho, Bw. Gilbert Grid licha ya kupongeza ujio wa Waziri kiwandani hapo, alisema kiwanda chao kitaendelea kufanya uzalishaji kwa kufuata kanuni na taratibu zote za mazingira ili kujiepusha na migongano na taasisi za serikali ikiwemo Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

”Kumekuwa na ufuatiliaji wa muda mrefu wa namna ya kusafirisha mabaki ya shaba (slime & slug) nje ya nchi ambako soko lipo, ujio wa Waziri ambaye amejionea uzalishaji na uwepo wa mabaki hayo ni hatua muhimu kwa kiwanda kwa kuwa yanapobaki hapa kiwandani tunakosa nafasi lakini pia tunakosa mapato kwa kuwa huko nje yanahitajika,’’ alisema Bw. Grid bila kutaja nchi zinazohitaji taka hizo.

Naye Meneja wa NEMC Kanda ya Mashariki, Arnold Mapinduzi amewataka wenye viwanda wanaotumia malighafi za vyuma chakavu kufuata taratibu ikiwemo kununua malighafi hizo kutoka kwa wenye vibali vya ukusanyaji na usafirishaji.

“Waziri ameelekeza mambo ya kufanya kwa upande wa kanda ya mashariki, lakini pamoja na hayo, tunawataka wenye viwanda kununua vyuma chakavu kutoka kwa wakusanyaji wenye vibali. Kutokujua Sheria haitokuwa kama kisingizio kwa yeyote atakayebaini kukiuka utaratibu huo,’’ alise Bw. Mapinduzi.












Comments

Popular posts from this blog

Mbeya agro-processors get 5 acres to build 50 industries

Tanzania praised for being keen on fertilisers going to farmers

Mavunde: TADB offered 1.8bn/- to nurture Farm Access