Zungu ataka ushauri wa kitaalamu kutatua mzozo kati hoteli za fukwe ya Dar
Na Abdallah Luambano, Dar es Salaam
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Zungu ameliagiza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuteua wataalam wa mazingira ili waeleze sababu halisi za uharibufu unaotokana na mawimbi makubwa na kuwa chanzo cha mzozo kati ya hoteli za Kunduchi na White Sand.
Waziri Zungu amewapa wataalamu hao siku
nne kuanzania jana na kuwataka wawasilishe taarifa yao kwake ifikapo leo..
Akizungumza mara baada ya kutembelea
fukwe ziliko hoteli hizo mbili mwishoni mwa wiki Waziri Zungu amesema
anaamini mabadiliko ya tabia nchi ndiyo sababu ya msingi
ya uharibufu wa fukwe na chanzo cha mzozo baina ya hoteli hizo.
“Mabadiliko ya tabia nchi yanapelekea
kuibuka kwa athari tunazoziona katika fukwa zetu. Kukabiliana na
hali hiyo tunahitaji nguvu ya pamoja kati ya Serikali, Sekta Binafsi
pamoja na wadau wa Mazingira kwa ujumla,’’ amesema Bw. Zungu
Amesema kuwa Serikali itaendelea kuweka
mazingira mazuri ili kuvutia wawekezaji ikiwemo suala la amani na utulivu
lakini akawataka wawekezaji kote nchini kuzingatia kanuni na sheria za
mazingira.
“Tusingependa kuwa sehemu ya
migogoro. Sisi kama serikali kazi yetu ni kuhakikisha amani na
utulivu pamoja na kuleta suluhu za kudumu na kuchochea uwekezaji
hapa nchini,’’ ameleza.
Waziri Zungu ametembelea eneo
hilo kwa sababu Wellworth Hotels & Lodges Ltd, wanamiliki Hoteli
ya Kunduchi, wamekuwa wakituhumu White Sand Hotel kwa kuongeza
tatizo la fujo za mawimbi kutokana na hatua za kuhami maeneo yao
dhidi ya mmomonyoko wa ardhi unaosabishwa na vurugu za mawimbi makubwa.
‘’Serikali ya awamu ya tano inawahitaji
wawekezaji katika sekta zote za uchumi, tusingependa migogoro iendelea kwa kuwa
inarudisha nyuma jitahada za serikali. Naitaka timu ya wataalum
kutoka NEMC kukutana na wawekezaji hawa na kutoa suluhisho la muda mfupi huku wakijiandaa
na suluhisho la kudumu katika kukabiliana na changamoto hiyo,’’ amesema Waziri
Zungu.
Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dk.
Samuel Gwamaka, amewataka wawekezaji kuwaajiri maofisa wa
mazingira ambao watakuwa wakifanya ‘environmental audits’ kila
mwaka. Tathimini hizo zitasaidia kueleza changamoto za kimazingira kwa kipindi
cha mwaka mmoja.
“Mzozo huu kwa kiasi kikubwa unatokana
na kukosekana kwa wataalamu wa mazingira ambao wangeeleza kitaalamu katika
repoti za mazingira za kila mwaka msingi wa mawimbi na uharibifu unaotokana
mawimbi hayo na tatizo kushughulikiwa kwa wakati. Jitahidini kuajiri maofisa wa
mazingira ambao watawasiliana moja kwa moja na NEMC kabla mambo
hayajaharibika,’’ ameeleza Dk. Gwamka.
Mwanasheria wa Wellworth Hotels &
Lodges Ltd, Bw. Saimon Nguka amemshukuru Waziri Zungu kwa kutembelea
eneo hilo, na ameiomba serikali kuendelea kutoa ushirikiano na kufanyia kazi
changamoto za kiuwekezaji.
“Tunakushukuru kwa ziara uliyoifanya na
kujionea hali halisi katika fukwe hii. Tunaomba mamlaka zote za serikali
kuitikia wito kwa haraka badala ya kuacha haya mambo tukayashughulikia sisi
wenyewe jambo ambalo linaweza kuleta migogoro isiyo ya lazima,’’ amesema Bw.
Nguka.
Ziara hiyo ya Waziri Zungu ni mwendelezo
wa Wizara yake katika kushughulikia changamoto mbalimbali za kiuwekezaji hasa
katika upande wa mazingira na kuhakikisha wawekezaji wanafuata kanuni na sheria
za mazingira hapa nchini.
Comments
Post a Comment