Christon boys wapongezwa matokeo mazuri kidato cha nne
Na Isdory Njavike, Kisarawe
Serikali wilayani Kisarawe, Mkoa wa Pwani imeipongeza Shule ya Sekondari ya wavulana ya Christon mkoani humo kwa kusimamia misingi ya taaluma na kuiletea sifa kufuatia matokeo mazuri ya kidato cha nne 2019/2020.
Akizungumza katika Mahafali ya Pili ya Kidato cha Nne ya Shule ya hiyo ambayo kwa taratibu za shule hiyo hufanyika mara baada ya matokeo, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kisarawe, Bw.Mtela Mwampamba mbali ya kuupongeza uongozi wa shule na kamati ya wazazi aliwataka wanafunzi kudumisha nidhamu na kuongeza zaidi juhudi ya kujisomea.
“Ufaulu huu ni mzuri na sisi kama serikali ya wilaya tumefurahishwa sana na matokeo yenu ya kidato cha nne. Tunawapongeza walimu, wanafunzi na wazazi kwa kushirikiana kuhakikisha wanafunzi wanasoma kwa bidii na kufaulu vizuri katika mitihani ya kitaifa,” alisema Bw.Mwampamba.
Alisema Sekondari ya Christon imekuwa ikifanya vizuri katika mitihani ya kitaifa kidato cha nne na cha pili na kuwa mfano mzuri katika wilaya ya Kisarawe na hivyo kuzitaka shule nyingine kufuata nyayo.
Kwa mujibu wa DAS shule hiyo mbali ya kuwa mfano wa kuigwa kitaaluma kiwilaya pia imekuwa ikishirikiana na serikali katika nyanja mbalimbali hata wakati wa kukimbiza mwenge Mwaka jana waliweza kugharamikia chakula na kuifanya wilaya hiyo kuwa ya
kwanza kimapokezi kwa mkoa wa Pwani.
‘’Nipende kuwapongeza sana Christon kwa namna ambavyo mmefanya vizuri katika Mtihani wa Taifa na kushika nafasi ya kwanza katika Wilaya yetu lakini pia namna inavyojitoa kushirikiana na Serikali katika Nyanja mbalimbali,’’ alisema Bw. Mwampamba.
Mbali ya hiyo alisema Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli imefanikiwa kuiunganisha wilaya hiyo kwenye umeme wa gridi ya taifa ambapo mwananchi inatugharimu shilingi 27,000 kuunganishwa kwa huduma hiyo.
‘’Wilaya yetu ya kisarawe inajumla ya vijiji 84, mpaka sasa vijiji 72 vimeshaunganishwa na umeme wa gridi ya taifa, vimebaki vijiji 12, ambapo usimamishwaji wa nguzo za umeme umeshaanza,’’ alisema Bw.Mwampamba.
Awali Mkuu wa Shule Bw. August Minja aliipongeza Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri wanayofanya katika kuhakikisha kuwa lengo la kujenga uchumi wa kati na viwanda ifikapo mwaka 2025 unatimia.
“Sisi kama Christon boys tumeshaanza kutekesa azma ya serikali kwa vitendo kwa kuwaandaa wanafunzi kwa ajili ya kujitegemea wawe na elimu ya ziada ukiachilia mbali ile ya darasani ambayo itatoamchango chanya kwa serikali pamoja na jamii kiujumla,’’ alisema Bw. Minja.
Bw.Minja aliwashukuru wazazi na walezi kwa kuwaamini kuwapa watoto ili wapikwe kitaalama na maadili ya kitanzania na kuahidi kuendelea kjutoa elimu bora na inayokidhi matarajio ya taifa.
“Tunaishuru serikali serikali ya Wilaya ya Kisarawe kwa kutupatia ushirikiano mkubwa wakati wote tunapohitaji. Ushirikiano wetu namajirani pamoja na shule mbalimbali wilayani hapa na mkoa kwa ujumla ni mzuri na tunajivunia,” alisema Bw. Minja.
Naye mwakilishi wa wazazi ,Bw. Assah Mwambene aliupongeza uongozi wa shule hiyo kwa juhudi wanazochukua kuhakikisha wanawajenga wanafunzi kitaaluma, kimalezi sambamba na maadili ya kiroho.
‘’ Mahali panapostahili sifa ni vizuri tukasema, kiukweli sisi kama wazazi tunashukuru uongozi mzima wa shule kwa juhudi zenu mnazochuku katika kuhakikisha mnatoa elimu bora na siyo bora elimu,’’ alisema Bw.Mwambene.
Comments
Post a Comment