NEMC yaeleza mafanikio ya kikosi kazi cha dharura

 


Na Paul Mahundi, Dar es Salaam

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesema katika kipindi cha miezi minne ya uhai wa  kikosi kazi cha dhararu  kero na malalamiko juu ya  uhifadhi wa mazingira vimepungua na Watanzania wamejenga tabia ya kuona mazingira yanatunzwa na kulindwa.

 Mkurugenzi wa NEMC, Dk. Samuel Gwamaka, ameeleza Jijini jana kwamba uanzishaji wa kikosi cha dharura  kinachofanyakazi  saa 24 umekuwa na manufaa kwa taifa kwa sababu wanachi wamepata mahali pa kupeleka taarifa na zikafanyiwa kazi. 

“Hapo awali kulikuwa na malalamiko mengi kuhusiana na utiririshaji wa maji taka kutoka  katika baadhi ya viwanda kwenda sehemu zisizohusika na wakati mwingine kwenye makazi ya watu. Lakini  baada ya kuunda kikosi hiki  kero zimepunguza sana hasa  kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam,’’ ameeleza Dkt. Gwamaka.

Amesema mbali na kudhibiti utiririshaji wa maji taka  kwenye maeneo yasiyoruhusiwa,  kikosi kazi kimesaidia kudhibiti uchimbaji wa mchanga kando kando ya mito, kuthibiti  uchafuzi wa kelele pamoja na ukataji miti kwenye maeneo yasiyoruhusiwa.

“Taarifa ambazo zimewasilishwa kwenye kikosi kazi  zimesaidia sana kuchukua hatua za kudhibiti uchafuzi wa kelele, ukataji miti katika maeneo yasiyoruhusiwa na uchimbaji wa mchanga kando kando ya mito jambo linalochochea  mafuriko  na ubomokaji wa kingo za mito,’’ ameeleza.  Tayari NEMC imezihimiza halmashauri za wilaya kuhakikisha vijana wanahamasishwa kuunda vikundi na kuvisajili ili uchimbaji mchanga uratibiwe na halmashauri zipate ushuru.

Amesema udhibiti na uimarishaji wa tabia ya usafi wa mazingira katika makazi ya watu na mito vimesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu, hasa katika maeneo yenye watu wengi kama Jijij la Dar es Salaam.

Dkt. Gwamaka amewashukuru wananchi na wadau wote wa mazingira  kwa kushirikiana  vizuri na baraza katika kufanikiisha  malengo yake. “Tunawaomba wananchi wazidi kutoa ushirikiano ili kwa pamoja tuyafanye mazingira yetu kuwa  bora na salama,’’ alisema.

Dkt Gwamaka amewakumbusha Watanzania kuzingatia Sheria ya Mazingira na Kanuni zake ili kuepuka migogoro ya kisheria inayoweza kutokea iwapo  sheria na kanuni  vitakiukwa na baraza likachukua hatua kwa wahusika.

“Baraza litaendelea kusimamia sheria na halitasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayekiuka  sheria na kanuni zake. Nawaomba Watanzania  wafuate sheria, kanuni na maelekezo yanayotolewa na wataalam wa mazingira ambao wanapatikana  karibu nchi nzima,’’ alisema.

Comments

Popular posts from this blog

Set aside land for investment, Kairuki tells RCs,district councils

Mkuu wa Mkoa Pwani asifu juhudi za mmiliki wa Makampuni ya Global Packaging na Wande Printing

17 projects to house 80,000 tonnes of crops being built