Wakulima waimwagia sifa BriTEN kwa tiba ya udongo


David Nawepa, Iringa

Shirika linalohudumia wakulima kuinua kupato chao la BriTEN limesifiwa na wakulima wakati wa kozi mahususi ya kuwafunza wakulima namna ya kutumia chokaa mazao kutibu udogo.

Akizungumza kwa niaba ya wakulima, Bwana Samuel Bangi, amewambia washiriki wa kozi hiyo kuwa awali wakulima walidhani kuchoka kwa udongo ni jambo la kiasili ambalo linatokea kwa sababu tu ya upandaji wa mimea wa mara kwa mara.  Kwa sababu ya imani hii, ameeleza,  matokeo yake wakulima waliendelea kuumia pasipokujua namna ya kujinasua.

 “Tulikubaliana na mavuno kidogo au kuyakosa kabisa kwa sababu hatukuja la kufanya na huku tunaumia,” amewambia  wananchi waliohudhuria hafla hiyo.  

Baada ya kuwaeleza wataalamu wa BriTEN, ameeleza Bw Bangi mwenye shamba la darasa  katika kijiji cha Mlingano,  jibu lilipatikana. 

“Hawa wataalamu kutoka BriTEN ndiyo waliotusaidia kujua ukubwa wa tatizo; walileta  vifaa vyao wakaupima udongo na kutuelez una tindikali nyingi.  Hivyo tukaanza kutumia chokaa mazao na matokeo yake ni mazuri.”

Mapinduzi haya katika kutibu udongo yamejitokeza katika ukuuji wa pato la wakulima kinyume na ilivyokuwa zamani.

“Mimi nimejenga nyumba mpya kutokana na mavuno mazuri niliyoyapata baada ya kuanza kutumia huu utaalamu mpya,” amesema Bw Bangi.

Naye Meneja wa Fedha na Uendeshaji wa Kampuni ya Dodoma Cement, Bw Thomas Kohi, amewahakikishia wakulima wa Tanzania kwamba kiwanda cha Dodoma Cement kina uwezo wa  kuzalisha  chokaa mazao inayohitajika kutibu udogo ulioathiriwa na tindikali.  “Hivyo msiwe na wasiwasi chokaa mazao ipo ya kutosha na imethibitishwa na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na tumepewa hati.”

Amewambia wakulima kwamba pasipo kutibu udongo ni kazi bure kuweka bidii katika kulima, kupanda na kutumia mbolea.

“Ni lazima udongo utibiwe kwa kutumia chokaa mazao hadi kufikia daraja la PH 7, ndipo mbolea itaanza kufanya kazi.”

Ameeleza kuwa kiwanda kina uwezo mkubwa wa kuzalisha chokaa mazao kwa wingi na kwamba iwapo mteja ataeleza mapema mahitaji yake kiwanda hicho  kinaweza  kuzalisha hata tani 100 kwa siku.

Amewahakikishia wakulima kwamba tani moja ya chokaa mazao wataweza kuipata kwa shilingi 120,000/-

Hadhara hiyo ilitokana na ziara ya kimafunzo kwa wakulima wa mahindi iliyoandaliwa  kwa pamoja kati ya Kituo cha Kuendeleza Kilimo Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini (Sagcot) na Kampuni ya BriTEN katika kijiji cha Kiponzelo, mkoani hapa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya BriTEN amesema kwamba amewaahidi wakulima hao ushirikiano zaidi na kwamba huu ni mwanzo wa kunufaika na ushirikiano uliopo.

“Tumekuwa karibu na wakulima hawa kwa muda mrefu.  Kazi yetu kubwa ni kuhakikisha wanaelewa fursa zilizomo katika kilimo,  hasa kilimo cha mahindi ambacho ni maarufu katika eneo hili. Kumekuwa na malalamiko ya kukosa mavuno ya kutosha.  Lakini baada ya kuupima udongo tukabaini una tindikali nyingi. Hivyo huu ni mwanzo tu;  tutawapa elimu na wakulima wa maeneo mengine ili tatizo hili liishe kabisa,” amesema Bi. Kaiza.

Amebainisha kuwa wameanza na wakulima wa kijiji hicho kwa kuwafunza namna ya kutumia chokaa mazao.  Baadaye, ameahidi,  wataendelea na vijiji vingine kwenye kongani hiyo ya Ihemi inayojumuisha mikoa ya Iringa na Njombe.
Naye Mkuu wa Maendeleo ya Kongani kutoka Sagcot,  Bi Maria Ijumba, amewaomba wakulima wajifunze namna ya kutibu udongo kwa sababu hilo ndilo suala la kwanza kabla ya kunza kupanda mazao.

“Afya ya udongo ndiyo suala la kwanza katika kupata mazao mengi na yenye ubora hasa katika zama hizi ambazo kilimo kimekua biashara… Udongo ukikosa afya hata tija katika mavuno inapungua,” amesema Bi. Ijumba.

SAGCOT ni waunganishi wa sekta binafsi na sekta ya umma katika kutambua fursa kwenye kilimo na kuongeza mnyororo thamani wa mazao ya mahindi, soya, nyanya, viazi mviringo na maziwa katika kongani sita zilizopo ukanda wa nyanda za juu kusini ikiwemo kongani ya Ihemi.

Kongani za Sagcot ni Ihemi inayojumuisha mikoa ya Iringa na Njombe, Mbarali (Mbeya), Sumbawanga (Rukwa), Ludewa (Ruvuma), Kilombero (Morogoro) na Rufiji (Pwani).



Mkurugenzi Mkuu wa BriTEN, Ms Joseffyne Kaiza, akisisitiza jambo
    wakati wa kuonyesha wakulima katika Kijiji cha Kiponzelo, 
Mkoa wa Iringa,  namna ya kuweka chokaa mazao
 katika ardhi ili kutibu tatizo la tindikali.
 Kushoto Na Meneja wa Fedha na   Uendeshaji wa Kiwanda cha
 Dodoma Cement, Bw. Thomas Kohi akisikiliza kwa makini.

Bw  Samuel Bangi (aliyesimama) akieleza wananchi waliohudhuria 
mafunzo ya kutumia chokaa mazo kutibu udongo jinsi wataalamu
wa BriTEN alivyowatoa katika taabu kupata mazao kidogo 
kutokana na kutumia ardhi iliyoathiriwa na tindikali nyingi.
 (Picha zote  na Hafidhi Kido)



Comments

Popular posts from this blog

Gold mine in Songwe wins ministerial praise for protecting environment

Tanzania praised for being keen on fertilisers going to farmers

NEMC warns on emptying effluent in built-up areas, flood waters