TADB yatoa 1.8bn/- kufanikisha uzalishaji kiwanda cha Farm Access



Na Paul Mahundi, Dodoma

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu,Bw. Antony Mavunde ameeleza jinsi Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ilivyofanikikisha uzalishaji wa kiwanda cha kutengeneza madawa ya mifugo cha Farm Access  kwa kutoa shilingi 1.8bn/-.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitembelea maonesho ya NaneNane  katika Viwanja vya Nzuguni Jijini hapa jana na kufika banda la Kiwanda, Waziri Mavunde alipongeza juhudi zinazofanywa Benki ya Kilimo na hasa kufanikisha maendeleo ya sekta ya viwanda ikiwemo kiwanda cha Farm Access kilichopo mkoani Dodoma.

“Naomba nichukue  nafasi hii kuipongeza TADB na uongozi wake kwa hatua stahiki na madhubuti kuunga mkono azma ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kujenga uchumi wa viwanda hapa nchini” alisema Waziri Mavunde.
Alisema benki ilitoa fedha kwaaji ya ujenzi wa kiwanda mpaka uzalishaji wake  kuhakikisha utengenezaji na upatikanaji wa kutosha wa madawa ya mifugo kiwandani hapo pamoja na kutoa ajira kwa vijana wa kitanzania.

 Hatua hii ya kufanikisha ujenzi wa viwanda vya kimkakati kama hiki cha Farm Access zitasaidia sana kupunguza changamoto za madawa zinazowakabili wafugaji na wakulima sambamba na kuchochea ukuaji wa soko la ajira, alisema.
Mbali ya kuvutiwa na bidhaa za kiwanda hicho, Waziri Mavunde alimhakikishia Afisa Mwandamizi wa Maendeleo wa Kiwanda,  Dkt. Simon Mphuru kuwa serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kujenga uchumi unaotegemea viwanda ifikapo mwaka 2025 na kuahidi kukitembelea kiwanda hicho siku chache zijazo.
 
“Juhudi kama hizi lazima ziungwe mkono kwani zinalenga kuongeza mapato ya serikali kupitia kodi na pia kuzalisha ajira kwa vijana wa kitanzania sambamba na  kuunganisha mazao ya wakulima katika mnyororo wa thamani” alisema.

Aidha, Bw. Mavunde aliitaka TADB kuendelea kushirikiana na mabenki washirika kwa kuwawezesha wakulima wa zao la zabibu kumiliki viwanda vidogo vidogo vya kuongeza thamani ya zao hilo.

“Hatua za makusudi zinazochukuliwa na TADB kwa wakulima wa zabibu zinapaswa kupongezwa na kila mpenda maendeleo wa nchi hii.Nina waomba waendelee kuwajengea uwezo na  kuwawezesha wakulima wadogo kumiliki viwanda vidogo vidogo ambavyo vitawasaidia kuongeza thamani ya zao hilo” alisema.
Kwa upande wake, Dkt. Mphuru alimweleza Waziri Mavunde kuwa kiwanda kitaendelea na uzalishaji na kuiomba TADB kuendelea kuwawezesha na kuwajengea uwezo wakulima wadogo ili kufanikisha azma ya  ujenzi  wa uchumi unaotegemea  viwanda.

“Tunaishukuru TADB kwa mchango wake mkubwa katika kuleta mageuzi na mafanikio katika sekta za kilimo na viwanda. Tunawahamasisha watanzania wengi kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo kwenye sekta ya kilimo”, alisema Dkt. Mphuru.





Comments

Popular posts from this blog

Tanzania praised for being keen on fertilisers going to farmers

Gold mine in Songwe wins ministerial praise for protecting environment

Kirenga: Kipaumbele chetu ni mkulima mdogo kupata soko la uhakika