SIDO yaibua viwanda 8,477 miaka 5 iliyopita

-->
Na Moses Mahundi, Dar es Salaam

Katika  miaka mitano iliyopita Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) limesimamia ujenzi wa  jumla ya viwanda 8,477 ambavyo vimeibua  zaidi ya ajira 500,000 jambo limechangia kukua kwa pato la taifa na kuifanya Tanzania kuwa taifa lenye uchumi wa kati.

Akizungumza katika mahojiano maalum kuhusu uhusiano wa dhana ya uchumi wa kati na mchango wa SIDO katika kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa kati jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa SIDO, Profesa  Sylvester Mpanduji,  ameeleza kuwa uchumi wa kati umefungamana mno na kuwepo kwa viwanda na kwamba SIDO imetekeleza kwa vitendo sera ya kuanzishwa kwa viwanda ili kufikia lengo la uchumi wa kati.

“Tumepata viwanda vikubwa 201, viwanda vya kati 460, viwanda vidogo 3406 na viwanda vidogo sana 4410 vimeanzishwa katika kipindi cha serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli na kuliwezesha  shirika kufikia asilimia 98 ya malengo yetu,” amesema Prof.Mpanduji

Viwanda vya ndani hurahisisha na kuborasha maisha ya watu na kwa kuibua  masoko ya malighafi,  bidhaa za viwandani  na ajira  na hivyo kupunguza umaskini wa kipato.

Prof. Mpanduji amesema soko endelevu na lenye uhakika ni soko la ndani ya nchi, na kueleza kwamba  SIDO inawahamasisha wazalishaji wa ndani  kuzalisha bidhaa zenye ubora ili Watanzania wapende kununua bidhaa hizo.  Amesema ni  kwa njia hiyo Tanzania itawaeza kuimarisha soko la ndani na kulinda viwanda vyake.

“Mteja anapenda kupata bidhaa bora kulingana na fedha yake. Hivyo ili viwanda ziendelee kuwepo lazima  ubora wa bidhaa uimarishwe ili kujenga imani ya wateja katika soko la ndani na hatua ya pili ni kuibua  fursa ya kupata masoko ya nje ya nchi,” ameeleza.

Amesema  ajira nyingi zimezalishwa na viwanda vidogo sana na viwanda vidogo na kufafanua kuwa sekta ya viwanda imechangia  asilimia 8.5 katika pato la taifa  mwaka 2019 na kwamba mchango huo wa viwanda umehamasisha na kuchochea maendeleo nchini.

“Uwekezaji katika sekta ya viwanda, hususani viwanda vidogo nchini , umeongeza uzalishaji wa bidhaa mbali mbali ikiwemo bidhaa za nguo na mavazi, ngozi na bidhaa za ngozi, kusindika nyama, chakula, mboga na matunda, maziwa, mafuta ya kula, sukari, vifungashio, mbolea, pamoja na viwanda vya kubangua korosho”, amesema Prof.Mpanduji

Ameeleza kuwa katika kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa Corona,  SIDO ilihakikisha viwanda  vinazalisha vifaa vya kujikinga na ugonjwa huo ikiwemo utengenezaji wa barakoa na vifaa vya kujikinga.

“Vita dhidi ya Corona imekuwa rahisi kutokana na kuwepo kwa viwanda vyenye uwezo ndani ya nchi  naupatikanaji wa bidhaa mbali mbali.  Hali hii imepunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi,” alisema Prof.Mpanduji  

Prof.Mpanduji amesema kuna ushirikianao katika ya SIDO na NSSF, VETA, Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi(NEEC) na Azania Bank katika kuwawezesha wananchi kupata mafunzo ya ujasiriamali na mikopo.  Mafunzo ni mikopo vitawawezesha wahusika kuendeleza biashara watakazoanzisha mara baada ya mafunzo.

“Katika ushirikiano huu tunawawezesha wananchi kupata mikopo kuanzia milioni 5 mpaka milioni 50 na milioni 50 mpaka milioni 500 kwa Riba ya Asilimia 13, ambapo muda wa mkopo huo ni mwaka 1 mpaka miaka 7,” alisema Prof.Mpanduji

SIDO inatoa mafunzo ya ujasiriamali na usimamizi wa biashara katika ofisi zake zilizopo katika kila mkoa nchini lengo likiwa ni kukuza ujuzi na kujenga ajira nchini.

Comments

Popular posts from this blog

Gold mine in Songwe wins ministerial praise for protecting environment

NEMC warns on emptying effluent in built-up areas, flood waters

Tanzania praised for being keen on fertilisers going to farmers